The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Sunday, 18 May 2025

nani kasema kitanda kinazaa haramu?


Kuna imani kuwa kitanda hakizai haramu. Uzoefu wetu unaonyesha kuwa kitanda kinazaa haramu japo uhalalishwa kwa visingizio mbali mbali kama mila, ujinga, na ubutu wa teknolojia. Ujio wa kipimo cha DNA unaonyesha kuwa kitanda kinazaa haramu tu.  Kusema kitanda hakizai haramu ni uchafu kimila. Ni hatari, majuto, na makosa makubwa kwa wasioamini wala kukubali uchafu huu kuoa au kuolewa kwenye makabila haya. Kwani, hawana uwezo wa kudumisha mila.

Tuanze na mfano wa Jerome (si jina lake) ambaye anathibitisha kuwa kitanda kinazaa haramu. Jerome ana siri iliyojificha kwenye mila chafu za kujamiana ndugu kwani, anafanana na babu yake kuliko baba yake. Pia, kuna minong’ono kuwa mama yake alipewa mimba na baba mkwe. Siyo siri tena kwa wanaomjua. 
        Kisa kingine ni cha Giloli (si jina lake) binti anayetoka kabila moja na Jerome. Tofauti, yeye ni mtoto wa kaka wa baba yake aliyezaliwa kwenye ndoa. Siri ya Giloli ilifichuka alipopata mchumba. Naye, hafanani na baba yake bali baba mkubwa. Alipochumbiwa, mchumba aliambiwa apelekwe kutambulishwa kwa baba mkubwa. ‘Baba’ yake aliishi mbali. Wanaojua, waling’amua na kufumbua fumbo lilojificha miaka mingi. 
        Jerome na Giloli wanatoka kwenye kabila lenye utamaduni wa kuchukuana ndugu kwa ndugu. Je katika jamii zetu wapo wangapi? Tafakari. Wakati ukitafakari, ujiulize. Ni watoto wangapi hufanana na baba zao wakubwa, wadogo hata wajomba hata majirani uliowahi kusikia habari zao?
Akiwa bungeni, Profesa Paramagamba Kabudi aliwahi kuwasihi Watanzania wasipime DNA za watoto wao. Fufuatilia clip hii. https://www.youtube.com/watch?v=sr3MZn9SMcE. Huu ni ushahidi wa kwanza kuwa kuna Jerome wengi kuliko unavyoweza kufikiria.
Kuna makabila na watu wenye tabia ya kuzaa watoto nje ya ndoa wakiwa katika ndoa au nadhiri hasa makasisi. Pia, zipo jamii zilizokubali na kuhalalisha jinai hii ambayo ni hatari kwa watoto na waliobambikiziwa. Katika makabila haya, watu hawa wako wengi, wanajulikana, na wengine wanakubalika chini ya dhana chafu ya kitanda hakizai haramu.
Je jinai hii husababishwa na nini? Kimsingi, zipo sababu nyingi kama vile ukosefu wa uaminifu katika ndoa, mila mbovu, tamaa, kutoweza kupata watoto wa jinsia fulani kwa baadhi ya wanandoa, kubakwa, uzinzi, na mengine mengi. Mila mbovu za ndugu kuchukuana ni chanzo kikubwa. Mfano, kuna makabila ambapo ndugu huchukuana kama mbuzi au panya bila kujali au kujua madhara ya kufanya hivyo. 
            Je utawajuaje? Utasikia kila baba anayekuja nyumbani ni ‘anko.’ Huu ‘uanko’ unaficha mengi.  Kuna makasisi wana watoto waliozaa na mahawara wao ambao huitwa anko na watoto wao wenyewe wa kuzaa. Watu na makabila haya yapo na yanakubali mila na tabia hizi chafu kama vile watoto wa babu na bibi mmoja huchukuana na hata wengine kuoana. 
        Huyu anamchukua mtoto wa baba mdogo, mjomba, shangazi, na wengine hata kuchukua wapwa zao ilimradi ‘wadumishe mila.’ Pia, kuna makabila yanayogeuza ndoa mali ya ushirika kwa kuruhusu baba mkwe au shemeji kumrithi mjane. Kama kurithi wajane ni jambo la kawaida, inashindikanaje wahusika kuchukuana hata kupeana mimba hata kabla ya kufiwa?
        Ikitokea mtu atokaye kwenye jamii isiyokubaliana na mila hizi chafu kuoa au kuolewa katika jamii hizi, lazima ataumizwa. Pia, watoto watokanao na dhambi hii huathirika kisaikolojia hata kiuchumi. Mfano mtoto ambaye baba yake halisi siyo mume wa mama yake, hawezi kumjua au kumfaidi mzazi wake. Hivyo, kijamii, anakuwa ametenganishwa na mzazi wake halisi na kuunganishwa na mzazi bandia. 
                Pia, inapotokea mzazi wake ana mali, hana uwezo wa kumrithi ukiachia kutowajua au kukua na ndugu zake. Pia, inapobainika, uwezekano wa kuvunja ndoa ni mkubwa. Hamjasikia visa vya baadhi ya wanaume kuua watoto wanasio wao au wanandoa wanaoua wenzao wagunduapo wamebambikiwa watoto? Je hapa kitanda hakijazaa haramu na jinai?
            Je nini kifanyike kuepuka unyama na utapeli huu? Tunashauri jamii zisifumbie macho jinai hii. Badala yake, tuelimishane madhara ya jinai hii kuepusha mateso kwa watoto, talaka, na vifo vyao hata wazazi wao. Hakika, kitanda kinazaa haramu. Kuweni macho.
Chanzo: Mwananchi leo.

Friday, 16 May 2025

Nitashinda urahis wa mafyatu kimiujiza na vishindo


Najua. Kaya yetu inafanya uchakachuaji, sorry, uchaguzi mwaka huu. Sambamba, nasi mafyatu tutafanya uchaguzi si uchakachuaji wa rahis wa mafyatu Mheshimiwa, Daktari, Profesa, ustaadh, Al haj, Muadhamu, Mtakatifu, Muona Mbali Fyatu Mfyatuzi. Hivyo, ili kujihakikishia ushindi wa kishindo na wa miujiza, nimeweka mikakati ifuatayo:
            Mosi, nitahakikisha nashinda hata kwa bao la kisigino watake wasitake. Mwenye wivu si ajinyongelee mbali.
             Pili, nitatoa ahadi kama sina akili nzuri. Lazima niwaaminishe mafyatu kuwa mimi ndiye ninafaa hata kama sifai. Lazima wajue kuwa bila mimi, watayumba na kuteseka sana.
Tatu, nitahakikisha wapingaji wenye kuonyesha ushawishi wanafunguliwa kesi za wizi wa kuku au za kubambikizwa. Pia, nitawaambia na kuwaaminisha mafyatu kuwa wanapaswa kuwaogopa wapingaji kama ukoma. Hii ni kutokana na ukweli kuwa wanatumiwa na ‘maadui’ wa mafyatu toka ughaibuni wanaotaka kuharibu amani, ulaji, na utulivu vyetu.
             Nne, nitaamuru migambo yetu kuwasweka ndani wote wanaoonyesha kutishia ushindi wangu. Hapa, lazima kusiwe na huruma, haki za mafyatu wala nini bali kufanya kweli kwa kuteka, kutembeza kipigo, na ikibidi kuweka ndani bila kutoa maelezo wala kufuata sheria za mafyatu.
             Tano, nimehakikisha mafyatu wananipitisha siyo kunichagua kama kanuni za katiba ya mafyatu inavyotaka kwenye kura za mchujo na uchaguzi wa ndani ya chata letu tukufu. Mafyatu wasenzi kweli. Si wapo waliotaka eti nipambanishwe na wanachama wengine wa Chama Cha Mafyatu (CcM) ili kupata mgombea anayekulika. Niliwazuia kutenda dhambi hii ya kunipambanisha mie mtukufu na watukutu katika chama chetu. Nani hajui kuwa mie napendwa na kukubalika? Anayebisha aulize miti, wadudu, hata wanyama. Mie nakubalika bwana. Anayeendelea kushuku hili, ajiulize ni kwanini nasifiwa kwa kila jambo hata lisilopaswa.
            Sita, nitahakikisha wakati wa kampeni hakuna kuwapa nafasi wapingaji wangu kufanya kampeni. Tena nitumie fursa hii kutoa angalizo na onyo. Yeyote atakayeshirikiana na wapingaji wangu ajue. Atakipata cha moto. Wao kama nani wafanye kampeni sawa nami wakati wanajua wazi mshindi ni mimi? Nani aruhusu wapingaji wavuruge amani na utulivu wa mafyatu? Mafyatu hawajui kuwa niliapishwa kulinda ulaji na si wao? Je huu siyo muujiza unaolenga kuleta amani na mshikamano chamani?
           Saba, kwa mjibu wa katiba ya CcM, mwenyekiti ana turufu ya kuteua wasimamizi wa wilaya na mikoa kama ilivyo kwa lisiri kali. Hivyo, nimewaamuru watendaji wangu wote kuhakikisha wanatumia mamlaka niliyowapa kuzuia upuuzi unaoitwa mikutano ya hadhara. Hii si mikutano ya hadhara bali ya madhara. Nani anapenda madhara wakati huu wa kusaka ulaji wa dezo tena mnene? Atayekaidi agizo hili ambalo, kifyatu, ni sheria, natengulia mbali uteuzi wake tuone kama atakula mafi yake nyambaff.
              Nane, nitaamuru vyombo vya umbea vyote vya kifyatu kutangaza sera zangu pekee huku vikihakikisha vinawabana na kuwakadia kwa kuwanyima fursa ya kutangaza utopolo wao wapingaji. Atakayekaidi na kutangaza ujinga wa wapingaji, ima nitamfungia au kumnyima matangazo ya biashara, au kufutulia mbali chombo chake nione kama atakula jeuri yake.
             Tisa, nitanunua na kupandikiza vyama pandikizi ili ‘vishindane’ nami ili kuhalalisha miujiza yangu katika kushinda uchakachuaji, sorry, uchaguzi kwa kishindo na miujiza vinafanikiwa. Viongozi wa vyama hivi lazima niwapige njuluku walainike na kujifanya wananipinga wakati game letu ni moja au siyo? Kwa usawa huu, bila kuja na mikakati kama hii, unaweza kuadhirika bure mzee mzima ukatupwa nje ya ulaji na kuchekwa hata kufunguliwa mashtaka kwa makosa ambayo nimeshafyatua. Nawajua mafyatu. Hawana akili nzuri wala dogo.
            Kumi, napanga uchakachuaji, sorry, uchaguzi uwe wa amani na utulivu. Hivyo, ili kuhakikisha hivi vinafanyika, migambo watatembeza kipigo kwa yeyote anayetaka kutishia amani na utulivu wa ulaji wangu na wapambe wangu.
             Kumi na moja, ili kuwaweka sawa mafyatu, nitaanza kuhubiri amani kwa kuwatishia na migogoro na vita vinavyoendelea kwenye kaya za mafyatu jirani. Lazima wajue kuwa bila mimi kuukwaa urahis, mafyatu wote watakabiliwa vita na matatizo makubwa. Kufanikisha hili, nitaamuru runinga zote za mafyatu kuonyesha madhara ya migogoro na vita husika. Kwa niwajuavyo mafyatu, bila kuwatisha, wanaweza kunitisha hata kutishia ulaji wangu mtukufu.
          Kumi na mbili, kuanzia sasa hadi uchakachuaji, sorry, uchaguzi, nitaanza kumwaga misaada kila mahali ili mafyatu wanichague. Najua. Walivyopigika, hawatatoboa. Pia, kwa walivyochelea kufyatuka wakafyata, hawatauliza hisani hii ni ya nini wala njuluku nitakazomwaga zimepatikanaje au nitazirejesha vipi. 
         Kumi na tatu, nitahakikisha mwanangu mwenyewe ndiye atakayesimamia wizara ya mafyatu inayosimamia mambo ya uchakachuaji ili tusije kupigwa bao la kisigino na wabaya wangu waliojazana kwenye chama chetu.
            Kumi na nne, nitaanza vita na mataifa yanayojifanya vijogoo na kutaka kutufundisha demokrasia na haki za mafyatu kana kwamba mafyatu wangu ni wao.
Du! Ndoto nyingine zikichanganyika na bangi ni balaa! Kumbe naota urahis siyo urais!
Chanzo: Mwananchi Jtano iliyopita.

Sunday, 4 May 2025

Fyatu afyatua figa na fwakit kuhusu Kanada

Tangu nifyatukie Kanada, nimekuwa nashuhudia mambo ya ajabu toka kwa mafyatu. Wapo wanaoomba mialiko ili waje huku wagome kurejea kwao na kufanya niwatunze hadi nifyatuke. Wapo wanaonipiga mizinga tena mingine ya kijinga siyo kifyatu. Hivi, unajisikiaje fyatu ambaye ameishastaafu kukubomu dolari 500 kwa ajili ya harusi ya kitegemezi chake na si kwa ajili ya matibabu yake? Akili au matope? Kwanini kuoa, kuoza, na kuozwa kwa mifuko ya mafyatu? Je wao walipooa au kuolewa uliwachangia lau moja ya kumi ya hizo unazoiitisha?
        Ajabu ya maajabu, siku hizi, mafyatu wanaweka hata kiwango cha chini cha nchango wa harusi kana kwamba wanajua una kiasi gani benki au uchagoni! Hakuna mafyatu waliokosa ubunifu kama wangu. Hata mamlaka zinahangaika na njuluku za madiaspora wakati haziwatendei yoyote zaida ya ntima nyongo. Ukitaka kujua huu ni ukumbaff, sorry, unyonyaji na uzwazwa, itisha nchango wa kupeleka kitegemezi shule au mgonjwa hospitalini, hawajachangii. You know what? Loo! Nimesahau naongea na mafyatu wa kibongo na si wa kitasha siyo!
        Hayo ya kimombo na watasha tuyaache. Ukichunguza nchango, wengi hawachangii harusi wala nini bali kupata fursa ya kula, kunywa, na kufanya mambo yao. Kwa mafyatu wanaopenda kudumisha mila, wanajua ninachomaanisha hapa au siyo? Wanajificha migombani na kumaliza mambo yao. Kwa ufupi, ni kwamba hawakuchangii harusi wala wewe bali wanajichangia kwa kisingizio cha kukuchangia. Ni ajabu. Wavyele wengi hawaipati hii. Chao ni kujisifu kuwa harusi ilinoga wakati yote ni malengo na mifuko ya mafyatu wasioona mbali. Kwanini hiyo njuluku mnayounguza kwenye utopolo kama harusi msiichangie kwenye kununua hisa hata kwenye masoko ya njuluku?
        Turejee kwa Kanada au Kanuki kama waiitavyo wenye kaya yao hasa wale originali siyo sisi wa nkorogo tuishio kwa vibali vya ukazi hata watasha walioivamia na kuitwaa na kuigeuza yao kiasi cha kutuuliza sisi nyie mwatokea wapi kana kwamba wao si wakuja kama sisi. Kanada ina ukubwa wa kilometa za mraba 9,093, 507 ikilinganishwa na Bongo yenye 947, 303. Hii maana yake ni nini? 
    Ni kwamba Kanada inaimeza mara tisa na nusu na ushei. Mkoa (Himaya) mkubwa kuliko yote Kanada wa Nunavut unaweza kuimeza Bongo mara mbili na ushei kwa ukubwa wa kilometa za mraba 2,093,190. Jiulize. Pamoja na ukubwa wote huu, ina mafyatu wangapi? Cheka taratibu. Ina jumla ya mafyatu 41, 414. Kama mafyatu wa Nanavut wakiamua kugawana himaya wao, kila mmoja atapata si chini ya kilometa 30 za mraba kama shamba lake ikilinganishwa na Bongo ambapo kila mbongo atapata kilometa za mraba 14. Kwa Visiwani, kila mmoja atapata 000.13!
            Shangaa sasa. Hata mkoa mdogo kuliko yote wa Kanada wa Prince Edward Island (PEI) yenye ukubwa wa kilometa za mraba 5,660 ni mkubwa kuliko Visiwani yenye ukubwa wa kilometa za mraba 2, 462 ambayo ni mara mbili na ushei? Je wajua kuwa Visiwani ni 1 ya 383 na ushei ya Bara? Ajabu, zote mbili zina haki sawa katika muunganiko! Ukiuliza mantiki, sijui kama utapata jibu lifyatualo akili zaidi ya siasa na sanaa. Katika siasa, moja na 400 ni sawa! Japo sina takwimu, ukweli ni kwamba wazenj wengi, kupitia mgongo wa muungano wa mnyonyano, sorry mpendano, wapo wengi bara kuliko visiwani. Ni udugu na upendo kiasi gani kiasi cha 1/383 kutoa hata mnene wa kaya? Du! Ningekuwa braza Mtikisa wa Tikisa gabacholi, ningeuliza. Je nani iko roga nyinyi ambaye nanyonwa lakini haipo fanya hesabu na hoji dugu yangu?
            Ukija kwenye pato la jumla la Kanada, ni Dola 37, 317 ikilinganishwa na Bongo yenye dolari 2,500. Hii maana yake ni nini kifyatu? Ina maana Mkanada mmoja ana uwezo wa kiuchumi mara 15 ya fyatu wa Kibongo. Ajabu, mafyatu wa Kikanada hawachangishani kwa ajili ya harusi. Je wajua Kanada ina idadi ya mafyatu wangapi? Jibu ni rahisi. Ina 41,528,680. Siombi msamaha kwa wale wanaochukia namba. Wapo waliodhani kuwa Fyatu Mfyatuzi hajui kuzifyatua namba kwa vile ni mwanasharia na mwandishi wa umbea. Kwenye namba, nilikuwa nampa taabu ticha wangu zama zile za ujima. 
        Wengi hawajui kuwa nina tuzo ya Nobo ya namba! Pia, nina tuzo ya juu ya takwimu. Nina uwezo wa kufanya mahesabu hata ya maji na uji na namna unavyoingia tumboni mwa mafyatu. Nina uwezo wa kuhesabu matone ya mvua na michanga ya bahari. Unadhani natania? Niulize michanga ya bahari au matone ya mvua ni kiasi gani. Hata usipouliza, acha nikupe jibu la kimahesabu kuwa ni mengi na mingi. Kkkk. Umenipata siyo?
            Una habari kuwa mimi ndiye niligundua formula ya mahesabu kuhusiana na idadi ya vitu. Mimi ni mgunduzi na mvumbuzi wa fomula ya ingi. Hivi, nimesemaje?
Chanzo: Mwananchi, Aprili 30, 2025.

Talaka na Madhara Yake


Tunajua fika kwa uzoefu wetu hata utafiti. Hakuna binadamu wala mwanandoa anayependa wala kushabikia talaka hata kama baadhi ya dini na sheria vimeiridhia kutokea ikilazimu. Hivyo, katika kipengee hiki tutajadili talaka na madhara yake hasa kwa wanandoa, familia, na jamii hata nchi kwa ujumla. Kwa vile siyo kila kitu kinaweza kutafsiriwa au kueleweka kwa mujibu wa kamusi, tutaepuka kuwachosha na maana au tafsiri za talaka kwa mujibu wa mamlaka mbali mbali kama vitabu vya kidini na vya kisheria. Tunaamini kuwa talaka, kwa lugha, nyepesi ni kinyume cha ndoa.
         Kwa ufupi, talaka ni kifo cha ndoa. Palipo na ndoa hakuna talaka na palipo na talaka hakuna ndoa na viwili hivi haviwezi kuishi kwa pamoja katika sehemu moja yaani ndoa kwa wakati mmoja.
Pia, ifahamike. Talaka, tofauti na ndoa, ina madhara makubwa kwa wanandoa binafsi, watoto, jamii na nchi. Mfano, chukulia mfano wanandoa wanaomilki mali kwa pamoja kama vile gari, nyumba, hata shamba. Wanapotalikiana, huwa maskini. Kwani, wakigawana mali zao, wanabakia watu wasio na vile walivyokuwa navyo kabla ya kuachana. Pia, ieleweke.
         Kuna vitu visivyogawanyika kama watoto ambao wazazi wakitalikiana, huwachanganyikiwa kwa vile ni vigumu kuwagawana wazazi au kugawana mapenzi yao kwao kwa usawa. Hapa, ndipo ilipo kadhia ya watalaka kuuana hata kuhujumiana kiasi cha kudhoofishana wao na watoto wao hata jamii. Zaidi, kesi za talaka hutumia muda na fedha nyingi kiasi cha kuathiri utendaji na uzalishaji wa wahusika. Hivyo, ndoa ni sehemu ya kutunza mafanikio ya wawili na hata jamii kwa ujumla mbali na kuwapa watoto kinga na utulivuv na mafanikio katika maandalizi ya maisha yao. Athari na hasara za talaka ni nyingi mno kiasi kwamba hatuwezi kuzielezea zote kwa ukamilifu katika kipengee kimoja. Cha msingi, ni kuiogopa, kuitahadhari, na kuiepuka kadiri iwezekanavyo. Kwani, haijengi zaidi ya kubomoa.
        Hata hivyo, upendo ukiwa wa kweli na kufanikisha lengo la ndoa, ni kinyume. Wahusika wataridhika, watafurahi, watafanikiwa, wataongeza upendo, na kuishi maisha marefu ikilinganishwa na walioharibikiwa au kutalikiana. Tunapoongelea madhara ya talaka kuhusiana na uchumi na mahusiano ya wahusika, hatugusii vifo vitokanavyo na kuachana. Kwa mfano, kwa mujibu wa National Library of Medicine (2022), takwimu za mauaji ya watalaka katika nchi ya Ufini, zinaonyesha kuwa kati ya 2003 na 2013, yapata 65% ya wanawake waliouawa nchini humo waliuawa na ima wenzi wao wa sasa au wa zamani iwe ni katika ndoa au mke na mume waishio kinyumba.
           Mwaka 2007 pekee, chini Marekani, wanawake wapatao 45% waliuawa na wenzi wao wa sasa au wa zamani. Hapa inaonyesha kuwa mauaji ya wanandoa yanayofanywa na wenzao ni janga la dunia na wahanga wengi ni wanawake. Hii haina maana kuwa hakuna wake wanaoua waume zao iwe ni wa sasa au wa zamani. Kwa mujibu wa jarida la Forbes (2024), idadi ya wanandoa waliouwa na wenzao ilikuwa 1,363 katika kila 100,000 kwa watalaka ikilinganishwa na 779 katika kila 100,000 kwa walio katika ndoa. Kwa mujibu wa Forbes (2024), talaka huathiri wanawake kwa viwango tofauti na wanaume. Mfano, wanaume huathiriwa na janga la ndoa kwa uwiano wa 1,772 kwa kila wanandoa 100,000 ikilinganishwa na wanawake 1,095 kwa kila wanandoa 100,000 Hapa somo ni kwamba kuna wanandoa wanaaendelea kuishi kwenye ndoa hatarishi hadi kuua au kuuliwa.
            Hali hii hatarishi inajenga maswali mengi juu ya ni kwanini watu waliokutana wakaamua kupendana na kuoana huuana. Japo hatuja jibu na sababu zote, tunaamini kuwa mauaji ya namna hii, ima yanatokanana kulipizana visasi, kuchanganyikiwa, hata kukata tamaa ya kuishi. Hivyo, namna ya kujiepusha na balaa hili ambalo linaweza kumkumba yoyote ni kujielimisha juu ya ndoa ili kulizuia hata kuliepuka. Kila gonjwa lina dawa. Na dawa ya kuimarisha na kufaidi ndoa ni kuielewa sawa na ambavyo tunapoumwa, huenda hospitali na kupata dawa na kupona ingawa si kwa magonjwa yote. Wahenga wanaasa kuwa ni heri kuzuia kuliko kutibu japo kutibu si vibaya ila kuzuia bado ni bora kwani humwezesha mhusika kuepuka baadhi ya magonjwa hata kifo.
Chanzo: Mwananchi J'pili jana.

Thursday, 17 April 2025

Napanga kuuza au kubinafsisha ubongo wangu


 

Sihitaji ubongo tena. Kwanza, umenifyatua nikafyatua wengine hadi wanatishia kunifyatua kwa kuninyotoa roho. Ubongo umesababishe kero na hatari hadi nikageuka machukizo ukiachia kujiudhi mwenyewe. Ubongo umenibomoa badala ya kujijenga. Nilifyatua wengine ili wafyatuke na kuwafyatua wanaowafyatua nikaishia kujibomoa. Mbali na ubongo kuniletea madhara kwa vile unachemka, zipo sababu zilizoko nje ya uwezo wangu zinazoniaminisha kuwa lazima niuuze lau nipate njuluku ya kupatia kanywaji. Zifuatazo ndizo sababu zilizonisukuma kuuza hata kuubinafsisha ubongo wangu ili niwe huru:
Mosi, siku hizi sihitaji ubongo. Wa nini wakati nina simu janja, kompyuta na gadgets nyingine ambavyo hufikiria kwa niaba yangu? Hapa sijaongeza akili mnemba (AI).
        Pili, nina wanasiasa wanaoniwakilisha kwenye vyombo vya kufikiri kama vile kunitungia sheria hata kama zinanikandamiza au hazinifai? Hawa waungwana, kwa kutumia bongo zao, wanafanya ubongo wangu uende likizo. Hebu fikiria. Kila ufikapo msimu wa kutengeneza kura za kula, wajanja hawa huja na kunihonga udohoudoho na udonodo mwingine tena kwa siku moja. Mie, huwapa kura ya kula kwa miaka mitano. Kwa ambao hawajajiandaa, msimu huu wa kulishwa ili kuliwa soon utaanza. Mafyatu kaeni chonjo saa mbaya.
        Tatu, nina viongozi wanaotenda miujiza kiasi cha kufanya maisha yangu yawe poa. Juzi nilimsikia mmoja akisema kuwa ukiona wanakopa na kuomba, jua ni wakwasi. Kwani, makapuku huwa hawakopi kwa vile hawaaminiki. Hakuna kilichonitisha kama upupu huu. Kama ni kweli kuwa kubomu na kukopakopa ni sifa ya utajiri na siyo sifa ya kipuuzi, inakuwaje kaya zinazokopa na kufadhiliwa zinaitwa kapuku? Kama fyatu kama huyu anapewa uongo, sorry uongozi, nini haja ya kuwa na ubongo unaoudhi kama wangu wa kifyatu? Lazima niupige seli kulalike.
        Kwa vile ninao viongozi tena wenye bongo zinazochemka, shahada za juu na maono, kazi yangu ni kutafuna na kusifia miujiza hii badala ya kupoteza muda kufikiri kiasi cha kutaka zaidi ya kile nilichopewa. Hivi kuku akianza kufikiri na kutamani kulala kitandani, amfugaye atamfanya nini? Je kuku akiwa na ubongo kama wangu akaanza kuhoji ni kwanini analishwa nafaka kavu na amlishaye anakura mayai yake yenye protein, ataishia wapi? Mnajua mfugaji tamfanya nini? Na akimfanya nini, atamlaumu aliyemfanya nini au ubongo wake?
        Nne, sihitaji ubongo kwa sababu baada ya viongozi wangu kutenda miujiza na kufanya maisha yangu kuwa swaaafi katika imani, siuhitaji. Kazi yagu ni kuimba mapambio na kusifia na hii ahihitaji ubongo bali utumbo. Kusifia hakuhitaji ubongo vinginevyo chawa wasingepata umaarufu kwa kufanya kazi hii isiyohitaji ubongo.
        Tano, sihitaji ubongo kwa sababu wengine niliowahusudu kama maprofesa walionifundisha wameonyesha wazi kuwa dunia ya sasa inahitaji usiwe na ubongo bali meno, maneno matamu na utumbo ndipo uuufyatue kabla haujakufyatua. Watoto wa kihuni huita kuukata. Ukiwa na ubongo, unakukata badala ya kuukata.
        Sita, kama ni masuala ya imani, ninao viongozi wa kiroho hata wenye uroho na roho mtakakitu hata kama nyingine ni za ajabu wanaoniombea kiasi cha kutohitaji ubongo kwa kazi yoyote ya Mungu hata shetani. Kwa vile dini yangu hainigeuzi kondoo ili wachunaji wanichune, sihitaji ubongo. Ubongo wa nini iwapo naweza kula na kunywa kwa miujiza na sara? Anayebishia ili, ajiulize ni kwanini watu wanapanda neno badala ya mbegu na kuvuna utajiri tena chapchap na hakuna mwenye ubongo anayehoji. Je hii siyo miujiza? Palipo na miujiza hapahitaji kuwa na ubongo bali imani. Na imani haitaki ubongo bali kukubali kila jambo hata kubadilishiwa jina na ubinadamu.
        Saba, lijapo suala la kupata njuluku, sihitaji ubongo ndiyo nizipate. Wa nini wakati, siku hizi, hata chawa anapata njuluku nyingi kuliko mchumi. Katika usawa huu ambapo wachumi wamegeuka wachumia tumbo, na utumbo unauzidi ubongo, ubongo wa nini wakati ukifikiri kwa tumbo unapata njuluku?
        Nane, nina uzoefu mkubwa wa kutumia ubongo kufikiri. Kwanza, kufikiri kunaumiza kichwa na hata kuuchosha mwili. Pili, kufikiri kunaamsha na kujenga tabia ya kuhoji na kupinga kiasi cha mwenye kuwa nao kuonekana mchokozi na mpingaji. Nani anataka ubongo ili autumie kujiumiza kwa kuhoji na kushuku hata kupinga wateule tena wa Sir God?
        Tisa, sihitaji ubongo kwa sababu kuwa na ubongo ni dhambi kuu katika mazingira ya jinai. Ubongo ni kiungo kidogo, kama mdomo, madhara yake makubwa. Unadhani bila ubongo, waandishi wa umbea wangebanwa kama wanavyobanwa na wenye mamlaka?
        Kumi, ukiwa na ubongo, unadai kila kitu na kukigeuza haki wakati wewe si mwenye haki. Kwa kutumia ubongo wangu, kuna kipindi nilijidanganya kuwa mimi ni mwenye kaya wakati wenyewe wapo. Baada ya kugundua walivyoniangalia na kutaka kunifyatua, niligundua kuwa dawa ni kuuza au kubinafsisha ubongo. Hivyo, usinishangae na kudhani nimefyatuliwa na mibangi hadi napanga kuuza ubongo. Je wewe unao? Du! Kumbe naota!
Chanzo: Mwananchi Jana.

Thursday, 10 April 2025

‘Niite’ Fyatu Mfyatuzi Nchonga Kambarange Nyerere

 


Juzi nilimsikia tapeli na zwazwa mmoja akijita kitegemezi cha mzee Nchonga (RIP). Ajabu, nasi mafyatu wake tuliufyata tukafyatuliwa utadhani huu si utapeli. Haraka haraka, niliwasiliana na Madaraka mwana mwenyewe wa Nchonga aliyewahi kunikaribisha Mwisenge nikahiji kwenye kaburi la baba wa kaya na kuniahidi kirungu. Ilikuwa ni baada ya kung’aka baada ya tapeli mmoja wa kisiasa aitwaye Washiti kupewa. Kwa busara na unyenyekevu, alinijibu “mwalimu alikuwa baba wa wote.” Kiakili, kifyatu, na kibusara, alinikata kilimilimi nikakubali yaishe. Pamoja na kuwa kitegemezi original wa baba wa taifa, Madaraka, huwa hapendi kujiita au kuitwa Nyerere zaidi ya Madaraka.
            Kwa kuangalia uhalisia na busara za Madaraka, inakuwaje matapeli wa kawaida tena wachovu na wachafu kujivisha ubini wa Nyerere nasi tunaangalia kana kwamba ni jambo dogo na la kawaida. Japo Nchonga ni dingi wa wote, hakuwa muasharati wa kuzaa nje ya ndoa yake. Hivyo, hata kama unampenda na kumheshimu kiasi gani, hupaswi wala huna haki ya kubeba ubini wake. Isipokuwa uwe fyatu kama mimi.
        Kwanza, kama wote tutabeba ubini wake, wabaya wake watasema tunamwabudia kutokana na kutupumbaza kiakili.
        Pili, tutakuwa tunawanyang’anya au kuwanyima vitegemezi vyake wa damu utambuliko na haki zao vya msingi.
        Tatu, watatokea matapeli hata maadui kutaka kumtumia ili wafanya upumbavu wao.
        Nne, tujikumbushe. Dingi wa kaya hakupenda kusifiwa wala kuabudiwa. Kwa wanaokumbuka, alivyowahi kusema kuwa, kidini, yeye aliuwa mwanaharamu kwa vile alikuwa mtoto wa mke wa tano.
 Hata huu utakatifu anaokaribia kupewa, kama angekuwa hai, ima angehoji hata kuukataa kwa heshima kuonyesha ubinadamu na unyenyekevu wake.
 Hivyo, badala ya kubariki iwe kwa kutojua au bahati mbaya utapeli na dharau kwa dingi wa kaya, tusimame imara si kukemea, bali hata kukomesha mara moja. Tusikubali kutumiwa kwa kuwaita matapeli waliojipachika ubini wa Nyerere kwa kuwaita hivyo. Bila kujua, tutakuwa tunaingizwa mkenge na katika kumtukana na kumdhalilisha dingi wa kaya. Vitegemezi vya dingi wa taifa vinajulikana viwe hai au kutangulia mbele ya haki.
            Tano, hakuna mfano wowote wa mafyatu wa kuvaa ubini wa kiongozi wao. Hata wakristo, walipewa ukristo na siyo ubini wa Yesu kwa vile hakuwa na watoto. Walivaa ukristo kama upakwa mafuta. Kuna kipindi maadui wa uislam toka ulaya walianza kuwaita waislam Mohammedans. Waislamu walichachamaa kwa sababu, a) huwa hawamwabudii Mtume Muhammad bali kumheshimu. Pili, wao si watoto wa Muhammad kwa vile Muhammad mwenyewe, kabla ya kufariki, aliwahi kuwaambia wazi kuwa yeye si baba wa yeyote bali baba wa watoto wake.
            Mbali na kuwa uzwazwa na utapeli, kujipachia ubini wa dingi wa kaya, ni ushahidi kuwa wanaofanya hivyo wameishiwa ubunifu. Wanaonyesha, kukopa maneno ya mwanafunzi wa Mwalimu, Benjamin Mkapa, kuwa ni wavivu wa kufikiri. Wanaonyesha wanavyotumia utumbo kufikiri badala ya ubongo. Niliwahi kuandika makala kuwakata watanzania kumuita rais Samia Suluhu Hassan hasa wale ambao wamemzidi umri waliomwitua maza. Hii ni kutokana na ukweli kuwa wanafanya hivyo kumdanganya, kumtukuza, na kutaka kumtumia mbali na kumzeesha. Kila mtu ana dingi na maza yake. Samia ana watoto wake na––––kama ilivyo kwa dingi wa kaya–––hana historia ya kuzaa kabla ya kuolewa au nje ya ndoa.
            Ukiachiwa kuishiwa na kukosa ubunifu mbali na utapeli, wengi wanaojifanya kubeba ubini wa dingi wa kaya, kwanza, hawana hata dalili moja ya kufanana nae mbali na kuigiza sauti yake au kujichora kama yeye. Kiusanii, tunawaruhusu wafanye hivyo. Kiuhalisia, hapana. Haiwezekani, ukamnasifibisha simba na panya. Pia, si vizuri walevi na vichaa kufagilia makaburi ya watakatifu. Ni ujinga wa pamoja, kuwaruhusu wazinzi kufanyia uchafu wao juu ya makaburi au majina ya mafyatu wetu maarufu waliopigania uhuru wetu.
        Juzi, niliona klipu ya mmoja anayejifanya kitegemezi cha dingi wa kaya akishindwa kusoma hata hotuba ya kimombo aliyoandikiwa. Nyerere alikimanya kimombo. Sasa inakuwaje anayemuingiza ni mbumbumbu na kihiyo? Ukimuigiza mtu, lazima ujitahidi ufanane naye ili kuleta maana na kuwasilisha ujumbe juu yake mbali na kuamsha kumbukumbu juu yake. Haiwezekani nune akamuigiza simba. Nune ni mdudu na simba ni mfalme na malkia wa pori. Kupe hata kwa usanii na utani, hawezi kubeba ubini wa tembo wala ng’ombe. Wawili hawa ni tofauti kabisa.
            Nimalizie kwa kuwaasa mafyatu tusikubali uchokozi wa matapeli, vilaza, na vihiyo wanatafuta riziki hata kwa njia chafu kuwachafua mashujaa wetu walioleta uhuru huu tunaofaidi na kuringia. Wote wanaojiita watoto wa Mwalimu Julius Nyerere wakome na kuacha ili kuwaachia watoto na família yao wafaidi haki na utambuliko wao. Japo hili linaweza kuonekana ni jambo dogo, madhara yake ni makubwa. Hivi nimesema naitwa Fyatu Kambaage au Nyerere?
Chanzo: Mwananchi Jana.

Monday, 7 April 2025

Umuhimi wa Wanandoa Kutunza Siri

Kuna busara wakati wa kuwafunda wanawali katika jamii moja nchini Uganda isemayo kuwa wanapoolewa lazima wajifunze kufunga miguu na kufungua macho badala ya kufungua miguu na kufunga macho. Hii hufanyika wakati mwali akijiandaa kwenda kwa mumewe. Wazazi hufanya hivyo kwa kujua kuwa nyumbani kwa mwali huacha kuwa kwao na huko aendako ndiko hugeuka kwake. Hamjasikia kwa Waswahili wakimwimbia bi harusi kuwa ‘sasa wenda kwako, utarudi huku kutembea?’

 Busara hii, licha ya kuzuia vishawishi vya  uasherati, inalenga kuwaambia wanandoa kuwa makini na waliowazunguka kuhusiana na maisha na ndoa zao. Inawahimiza kuchambua mambo na kujua ya kusema na ya kutosema. Siyo kila jambo lazima lisemwe au kuwekwa wazi kwa wasiohusika. Tumeshagusia kwenye kitabu cha kwanza namna mashoga wanavyoweza kuvunja ndoa. Pia, tuligusia juu ya imani au ushauri visivyofanyiwa utafiti vinaweza kuvunja ndoa. Ndoa nyingi zimevunjika na nyingine zitavunjika kwa sababu hizo. Hivyo, kama njia ya kuwafunda vijana, tumeamua kuchagua kisa hiki kufikisha ujumbe na ujuzi kadhalika.

            Kuna kisa cha mama tulichosoma kwenye gazeti moja la nchini Zimbabwe. Kisa hiki ni juu ya mwanandoa mwenye majivuno na asiyetunza siri za ndoa yake. Akiwa amekwenda kusuka nywele kwenye saluni, alizoea kumlaumu mumewe kwa wenzake kuwa alikuwa akimwachia pesa kidogo. Maskini, kayaya huyu hakujua kuwa alichoona kidogo, kilikuwa kikubwa kwa wenzake. Hivyo, baada ya kuwa akijisifu kwa kumsimanga mumewe kwa ‘kutomwachia’ pesa nyingi, walitokea waliotamani wangeolewa naye wakaanza kumuandama hadi ndoa ikavunjika na  mhusika akashangaa kujikuta aliyechukua nafasi yake alikuwa ni  mmojawapo wa mashoga yake aliyezoea kumlalamikia juu ya tabia za mumewe. Kimsingi, huyu mama hakufunga miguu na kufungua macho. Alipaswa afunge mdomo na kufungua masikio. Je ni wangapi wameishashuhudia au kukutwa na haya? Je hapa utamlaumu nani kama siyo wewe mwenyewe? Huwa tunawashauri na kuwahimiza wanandoa kutofanya maisha yao au ndoa zao magazeti au matangazo.

            Je ni wangapi hufunga miguu na kufungua macho au kufanya kinyume? Je hili halina faida kubwa kwao kama watalishika, kulikumbuka na kulitekeleza?   Unaweza kujisikia raha kuwasimulia wenzako juu ya maisha yako bila kujua madhara yake. Hata hivyom si wasikilizaji wako wote hujisikia kama unavyojisikia. Hivyo, si vibaya kushauri na kusisitiza kwa wanandoa kuchambua na kujua ya kusema na kutosema. Tunajua kuwa si wote wanapata bahati au kuwa na desturi, mila, na tamaduni za kufanya hivi hasa wakati huu wa utandawazi ambapo vijana wanaweza kukulia mbali na jamii zao hadi kuoa au kuolewa. Hivyo, kwa kuliibua na kulikumbushia hili, tunalenga kuwasaidia wasio na fursa au walio nayo lakini wasizingatie.    

            Wewe na mwenzi wako ni sawa na kata na mtungi. Siri ya mtungi apaswaye kuijua ni kata tu. Hivyo, unapofungua mdomo ukaziba masikio, utaumia tu taka usitake. Kama hujaumia, ni suala la muda na si kama bali lini utaumia. Pia, ni vizuri kubainisha kuwa unapaswa kujua mambo ambayo ni siri na siyo siri. Kama hujui, acha kuongea kabisa ili usijikute ukivujisha siri ukidhani siyo siri wakati ni siri. Kwani usiposimulia juu ya maisha yako utakosa nini ikilinganishwa na kuyasimulia ukaishia kujuta? Hata habari huwa hatuzipati bure. Ima utanunua chombo cha habari kama gazeti, runinga, au redio ndio uzipate au ulipie kwa wanaozitoa. Mbali na majanga na misiba, hakuna habari za bure duniani hasa wakati huu ambapo kila kitu ni bidhaa inayoweza kutumiwa na baadhi ya watu kutengeneza faida hata kama ni kwa hasara ya au kuwaumiza wengine.

            Turejee tulikoanzia. Mbali na kushauriwa ufunge miguu na kufungua masikio, tuseme wazi. Je unakosa nini usipofichua siri zako? Je unapata nini unapozisambaza? Kwani, lazima kila unachofanya wakijue watu wakati hujui wafanyayo? Hata ukiyajua wafanyayo, kwani lazima uyafahamu kwa kuhatarisha maisha, ndoa, na siri zako? Hivyo, usikubali kuwa habari kwani si kila habari ni nzuri. Waandishi wa habari husema heri upate habari kuliko wewe kugeuka habari.

Chanzo: Mwananchi J'pili.


Saturday, 5 April 2025

Wamefyatuka wanafyatuana mbele ya mafyatu!


Juzi tilishangaa sana. Mwe! Nani angeamini kuwa mafyatu wanene na wanono wangefyatukiana na kufyatuana hadharani? Unene kweli taabu japo una raha ya kula bila kutoa jasho! Si fyatu mmoja aliyekaribu na mwenyewe kapwakia ulaji kiasi cha kuanza kuwapayukia walaji wa chini yake wasio na nasaba na mwenyewe! Fyatu huyu mwenye kutia shaka, inaonekana, hagusiki. Nani anaweza kumgusa Keinerugaby Mwana wa Mu7 pale jirani? Nasikia shemela zake nao wanafyatua ulaji simply because wanashea bedrooms na vitegemezi vya Mu7. Haka kaugonjwa kanaanza kuenea. Ukiachia mbali Mu7, Jake Zoomer wa Bondeni aliwahi kuruhusu kitegemezi chake kiitwacho Insectzane kutumia maulaji yake utadhani ufalme. Pale kwa Nyayo ya zamani, Billy Rootor na vitegemezi vyake ndo usiseme. Vinafyatua kama havina akili nzuri. Hali ilikuwa chafu hadi ikawapo ofisi ya first daughter. Mafyatu wa k ule walishupaa ikafyatuliwa mbali.
                Nchini Equatorial Guinea, kitegemezi cha mdingi ndiye makamu wa dingi yake. Wakati kaya ya jirani karibu na Diarasee, kitegemezi cha mdingi kinafyatua njuluku kama za dingi wake. Kule Gabon, kitegemezi cha king’ang’anizi aliyefyatua na kuibia kaya ile kwa zaidi ya miaka 40 kilifyatua maulaji baada ya dingi kufyatuliwa na Sir God mwenyewe. Hata hivyo, nacho kilifyatuliwa na geshi kikaishia kuuona unene runingani. Kule Tchad na Togo, bado vitegemezi vinatesa baada ya midingi yao kufyatuka na kurejesha namba.

Nirejee kayani. Japo si kwa sana ikizingatiwa kuwa Stone hakuendekeza ujinga huu sawa na Nchonga na Brother Ben Nkapa. Kamchezo ka kupeana ulaji kiukoo kanaanza kugeuka donda ndugu. Ajabu, mafyatu wanachekelea badala ya kufyatuka wakafyatyua hawa wanaowafyatua! Leo sifyatui majina ya mafyatu fyatuzi wanaofyatuana baada ya kuwafyatua mafyatu nikaishia kuchengetwa kama siyo kufyatuliwa au kuzuiwa ili nifyate. Natamani niorodheshe vitegemezi vya wanene vinavyofyatua mafyatu just because of their surnames. Wengine hata hawana surnames nene bali za madingi wa washirika wao wa bedroom kama aliyefyatuka juzi akamfyatukia fyatu mwenzake mbele ya mafyatu jamaa anayesifika kwa kufyatuka na kupayuka bila kichwa kuwasiliana na midomo.

Brother Al Chakumila upo hapo? Nilijisikia vibaya dogo fyatu wa mwenyewe alivyokufyatua mbele ya mafyatu asijue anaweza kuwafyatua wakafyatuka na kufyatua. Je kipindi hiki utapona kweli? Ilikuwajekuwaje ukamgusa pabaya fyatu wa mwenyewe? Umesahau ulivyopayuka ukafyatuliwa na kukaa pembeni hadi mwenye alipokuhurumia akakurejeshea ulaji unaoanza kudodesha? Inaonekana ufyatu umeanza kukuzidi hadi unajifyatua na kuishia kufyatuliwa. Kwanini hujifunzi au huna kumbukumbu? Ungejua namba unazocheza nazo, wala usingejifyatua ukaishia kufyatuliwa ukafyata. Umewapayukia wengine usijue duniani malipo ni hapa hapa. Sasa ona umefyatuliwa tena hadharani na unafyata. Ingekuwa mie, kwa ufyatu na ufyatuzi wangu, mbona nshajifyatua na kuachia ngazi zamani gani.

Kuna kamsemo kuwa madaraka hulevya chakari. Yakishakulevya, unapoteza uwezo wa kufikiri, kujifunza, kukumbuka, hata kuona na kukubali ukweli. Sijui kwanini mafyatu hawataki kujifunza toka kwa mafyatu waliotesa kama akina Nebukanezza, Mchonga, Jiwe, na wengine! Kufyatukiana na kufyatuana hadharani si uongozi bora bali bora uongo na uongozi. Inaboa na kukera my friends. Japo mafyatu waligoma kufyatua, angalieni msifyatuane mkaishia kuwafyatua wakawafyatua bila kutarajia.

Japo brother Moody alipomfyatua na kumfyatukia brother Al, alikuwa na pwenti, kwanini wasikutane faragha wakayamaliza au ni yale ya kutafuta ujiko wasijue wanavifua na kufuana nguo hadharani bila sababu za msingi. Huwezi kuruhusu ndinga zipitie kwenye uwanja wa mapipa hata kama una power. Huu siyo uzembe bali ni hatarishi kwa madebe na ndinga mbali na abiria. Inakuwaje kayani kila fyatu anajifanyia atakavyo kana kwamba hakuna sharia na miongozo? Huwa nashangaa kusikia eti mkuru wa uilaya anazuia say mikutano ya hadhara kwa vile wanaoiitisha ni wapingaji. Kwani wapingaji si wanakaya na wapo kinyume cha katiba? Mnamfyatua nani kwa kujifyatulisha? Mkifyatuliwa, mnaanza kulalama kama vichanga wanapofyatuliwa kutokana na ufyatu wao uchwara.

Sasa ufanye nini? Nakupa ushauri wa dezo. Achana na kufyatukafyatuka na kupayukapayuka hovyo. Utafyatuliwa. Shauri yako. Usijesema sikukuonya. Unene wa kupewa si unene kitu. Wapo wanaoulinda wakilala na kuamka wakiota ni jinsi gani waanzishe kwaya za sifa ili ulaji usiwatoke. Wapo ambao wako hata tayari kukufuru ilmradi waendelee na ulaji.

Hakuna fyatu anayenifurahisha hata kama sifurahi kama yule aliyefulia. Jamaa likifungua domo kufyatuka ni makufuru na sifa. Mara mwenyewe katenda miujiza, mara kavunja rekodi, mara hivi, mara vile ilmradi siku ziende na ulaji na ukamuaji viendelee. Kwa tunaojua haya mambo na dynamics zake usawa huu, unatumia busara ya Kijamaika isemayo play fool to catch wise. Ukijitia kujuajua na kufyatukafyatuka ukapayukapayuka, unafyatuliwa na wengine wanatesa. Nakushauri utafute the 48 laws of power upone. Hivi nshaamka usingizini?

Chanzo: Mwananchi J'tano iliyopita.

Wednesday, 26 March 2025

Tusichachawe, kuchawishwa, tukachawishana

 

Kuna usemi wa hovyo. Kila nikiusikia, natamani nifyatuke na kuwafyua wadudu hawa wawe ni wadudu au ngurumbili waliofilisika kimawazo hadi kuwa hivyo walivyo hovyo. Msemo unaonichachefua na kunifyatua si mwingine bali ule wa chawa na uchawa ambapo chawa wenyewe ni mafyatu. Mwanzoni, nilidhani chawa wamepata miujiza kiasi cha kufyatuka kama mafyatu na kugeuka mafyatu lakini si mafyatu kufyatuliwa hadi wakajigeuza au kugeuzwa chawa. 
Kwanza, siamini wala kukubali kuwa fyatu mzima na akili zake anaweza ima kujifanya, kufanywa, kujiita, kuitwa, kugeuzwa au kujigeuza chawa. Chawa na fyatu wapi na wapi na katika nini na lini na iwe nini kwa ajili ya nini na nani? Fyatu mwenye akili timamu hawezi kuvumilia achia mbali kufuga chawa. Sijui kama chawa wana akili au ubongo hata uwe kiduchu kiasi gani. Sijui hata kama wana utashi au utambuzi wa kujua wafanyacho zaidi ya kusukumwa na silika kama hayawani wengine kama wao.
Chawa anapoitwa fyatu ni poromosheni na fyatu anapoitwa chawa si dharau na matusi tu bali demosheni. Kwanza, sijui. Inakuwaje fyatu mzima akubali kuitwa au kuita wenzake chawa asione aibu wala kuhofia kuonekana hayawani na zwazwa. Inabidi nirejee kwenye kabrasha langu la mabuku ya saikolojia nijikumbushe kitu hii.
Tofauti na chawa, kazi ya mafyatu ni kufyatua kila kitu, fyatu, na chawa bila kujali ukubwa wala unene wao. Hivyo, siamini hata kidogo kuwa fyatu mwenye akili timamu anaweza kuchawawishwa na kuchachawizwa hadi akakubali kuwa au kugeuzwa chawa. Ili iweje? Ili apate nini? Hata kama mie ni fyatu, lazima niseme tena bila kufyatuka. Hakuna binadamu anaweza kuwa chawa wala chawa kuwa binadamu. 
Kuwa, kufanywa, au kuitwa, kugeuzwa hata kuihisiwa kuwa chawa ni kufuru na maudhi kwa mwenyezi Mungu mwenyewe na mafyatu hata wadudu. Ni hayawani na vichaa pekee wanaweza kunyonywa na chawa kwa vile ni hayawani. Hawana uchaguzi wala uwezo kama mafyatu. Sitaki kufikiri. Sijui inahisika au kuwa vipi kwa fyatu kujilinganisha au kugeuzwa hayawani kama mdudu chawa. Sitaki kujua wala ku-imagine.
Kwa wale waliokua na kwenda shule wakati wa Ujamaa, tuliozoea kuwaita wanyonyaji kupe, si kwa sababu ya ufyatu wao bali hatari, madhara, uchafu, udhalili, na uhovyo wao. Tofauti ni kwamba, mafyatu wanyonyaji walipoitwa makupe, hawakupenda tusi hili. Nasi, tuliwaita vile si kwa kuwasifu wala kutaka watusifu bali kuwakatisha tamaa waache ukupe au unyonyaji. 
Kuna tofauti gani kati ya uchawa na ukupe? Kama wahusika wanamaanisha chawa kwa sababu ya unyonyaji na uchafu wao, hapa sina neno. Nijuacho, hakuna kupe waliojitangaza kuwa makupe au sisi tuliowaita makupe kuwavumilia na kuwafanya sehemu ya maisha au harakati zetu. Tuliwachukia. Walituchukia. Tulichukiana. Je kwa chawa hali ikoje? Mie si chawa. Sijui chawa wanajiteteaje kama wanao utetezi kutegemea na uteuzi wao.
Je ni kwanini tuliwachukia kupe? Nani anapenda kunyonywa? Nani anapenda kufuga viumbe visivyo na faida bali hasara na hatari? Wale watunzao wadudu wanyonyaji hufaidikaje nao? Je kunyonywa kuna raha au karaha? Nani anaweza kufuga maradhi kilio kisimfichue? Ni mpumbavu gani huyo anayengoja kufichuliwa na kilio badala ya kutibu ndwele? Wanyama kama ng’ombe, nyati, tembo na wengine hunyonywa na kunguni. Kwanza, ni kwa sababu wao ni wanyama. Pili, hawana dawa na nyenzo nyingine za kuwaangamiza japo wana utashi. Tatu, wana damu nyingi kuliko mafyatu. Nne, pamoja na kutokuwa na dawa na nyenzo, hawawapendi kupe.
Turejee kwenye chawa au machawa kama wasemavyo watoto wa njini siku hizi. Nina swali. Je chawa anaweza kuishi bila ya kuwanyonya awanyonyao? Je anayenyonywa anaweza kunyonywa bila kuwa na damu na uchafu, bila kusahau ujinga au kukosa uwezo kabisa wa kuwateketeza wadudu kama wanyama hapo juu? Je sasa nani hawa wanafuga machawa na kwa nini ili iwe nini? Je chawa wanaweza kuwapo bila damu na uchafu? Je nani hawa wachafu wanaofuga chawa na ili iweje? Kuna haja ya kuwasaidia ima kuwaosha wawe safi na kuachana na mateso ya kunyonywa na aibu ya kuitwa wafuga chawa au kuwapulizia dawa ya kuua wadudu kama tufanyavyo kwa mbuzi na ng’ombe ambao huwa tunawapelekea joshoni mara kwa mara.
Kimsingi, fyatu anayekubali kunyonywa na chawa bila kuwaua au kujisafisha, anahitaji msaada sawa na chawa wanaomnyonya. Unachoweza kufanya hapa, ni kuua machawa ima kwa kumuosha mhusika, kusafisha nyumba yake huku mkimfundisha faida za kuwa safi na madhara ya kufuga chawa au kupulizia dawa za kufyatua wadudu. Je anayefuga chawa na chawa nani mjanja? Je kati yao, nani anahitaji ukombozi? Kumbe nililewa na kulala kwenye mtaro!
Chanzo: Mwananchi leo.

Monday, 24 March 2025

Shemeji, huwezi kumpiga mke wangu


Kisa hiki kinamhusu rafiki yetu. Siku moja, rafiki yetu alisimulia kuwa kulikuwa na mabishano juu ya suala la kifamilia baina ya mkewe na kaka zake wawili ambao ni mashemeji zake. Katika ubishi huu, mke wa jamaa aliwapinga kaka zake juu ya jambo fulani kiasi cha kuwaudhi. Mmojawapo wa wale makaka ambaye ni mkubwa kwa kufuatana na mke wa jamaa alimtishia dada yake kuwa angeweza kumpiga. Kwanza, alisahau kuwa, pamoja na kuwa dada yake, alikuwa mke wa mtu. Pili, alisahau kuwa jukumu walilomkabidhi shemeji mtu alipomuoa dada yao ilikuwa ni kumlinda na kumtunza dhidi ya hatari au tishio lolote. Tatu, hakujua au alijua lakini akasahau kuwa shemeji yake alimpenda na kumheshimu sana mkewe kiasi cha kutoweza kuvumilia kuwa shahidi wa udhalilishaji au utesaji wake.
            Kaka mtu alipomtishia dada yake kuwa angempiga, shemeji mtu aliamka kwenye kiti pembeni ya mkutano wa ndugu na kumwambia shemeji yake “huwezi kumpiga mke wangu nami nikuache. Tutapigana liwalo na liwe.” Kwa vile wale wakaka hawakutegemea kitu hiki, walishangaa na kuogopa kiasi cha kuwataka radhi dada yao na mumewe na ugomvi kuishia hapo. Baada ya tukio hili, kaka mtu walimheshimu dada yao kiasi cha kuwa wakisimulia kisa kile mara kwa mara kwa kuangua vicheko.
            Kwa mujibu wa mtoa taarifa, kaka mtu walizoea kusema kuwa mumewe alikuwa amemfundisha kuwa na roho ngumu, yaani ugaidi. Kwani, hawakutegemea kuwa shemeji yao angeonyesha hasira na kuamua kuingilia ugomvi wa kifamilia. Badala ya kukuta ndugu wakigombana na kuchukua jembe akalime kama wahenga watuhusiavyo, mume mtu aliamua kuingilia kati akimkingia kifua mkewe. Jambo hili liliwapa somo kubwa wahusika. Kadhalika, jambo hili linatoa funzo kwa wengine kuwa, kama utamlinda mwenzio, hakuna atakayehatarisha maisha yake kwa kuwa tayari kumdhuru. Isitoshe, kama mke au mume ni mwili mmoja, kama mmoja atadhalilishwa au kupigwa, na mwingine, kadhalika atakuwa amedhalilishwa na kupigwa.
            Jamaa alitwambia kuwa baada ya mkasa kusuluhishwa hivyo, mashemeji zake walizoea kumuuliza ni kwanini aliamua kuingilia ugomvi wa ndugu badala ya kuchukua jembe akalime? Aliwajibu kuwa, kama angelaza damu na mkewe akadhalilishwa au kupigwa, angeenda kulipia nyumbani mbali na kushindwa kumlinda na kumheshimisha mkewe. Hivyo, alizoea kuwajibu kuwa walipompa dada yao amuoe, walikoma kuwa na mamlaka juu yake. Kwa maana nyingine, wahusika siyo walitaka kuwadhalilisha na kuwaumiza hawa wawili tu bali kupora madaraka ya shemeji yao. Je ni wangapi wanaliona hili hivi kiasi cha kumhami wenzi wao kama alivyofanya jamaa huyu? Ni wangapi wangechukua majembe na kwenda kulima wakati wakiacha mambo ya familia kama yalivyo japo aliyekuwa akiumizwa ni mke mtu? Je wewe ungefanya nini katika hali hii? Je hili limewatokea wangapi na walichukua hatua gani? Si vibaya kumlinda na kumhami umpendaye hasa anapokuwa mke au mumeo. Tuna wajibu kwa wenzetu kama walivyo nao kwetu pia.
            Hivyo, unapokutana na changamoto au tishio kama hili, wala usisite wala kuona aibu kumhami mwenzio. Kwani, kumhami ni wajibu wako na kutomhami ni kushindwa kutekeleza wajibu wako kwake na kwako. Hisani, siku zote, huanzia nyumbani. Kupenda siyo kuambizana nakupenda bali kuonyesha upendo kwa matendo. Hata sheria nyingi ziko wazi kiasi cha kuzuia mke kuwa shahidi dhidi ya mumewe. Chini ya kile kinachoitwa spousal testimonial privilege au haki ya ushahidi wa mwanandoa dhidi ya mwenzake, mwanandoa ana haki ya kukataa kutoa ushahidi dhidi ya mwenzie. Hata hivyo, sheria hii humpa haki haki hii mwanandoa kwa makosa yaliyodaiwa kutendeka wakati wakiwa katika ndoa si kabla au baada ya kuachana. Sheria, mara nyingi, ni kipofu na haina huruma. Ila katika kuleta amani katika ndoa, inatoa haki hii kwa wanandoa. Hivyo, wanandoa wasiojua sheria wasilazimishwe kutoa ushahidi dhidi ya wenzi wao kwa vile jukumu lao ni kulindana na kuhamiana katika kila hali. Pia, kumhami au kumlinda mwenzi wako si hisani kwake bali wajibu wako kwake.
Chanzo: Mwananchi, Machi 16, 2025.

Tulifyatuliwa, tunafyatuliwa, tutafyatuliwe tena

Mwaka jana, Mkaguaji mkubwa wa njuluku za sirkal aka KAGO alitoa taarifa ya kuchefua baada ya baadhi ya mafyatu kufyatua mafyatu wote waliokataa kufyatuka wakafyatua wapigaji wakaishia kuufyata. Alionya kuwa, kama ufyatuaji unaoendelea usipofyatuliwa, kaya nzima ima itaendelea kufyatuliwa kama inavyofyatuliwa na itakavyofatuliwa kiasi cha kufyatuka na kuanza kuwafyatua wanaoifyatua. Na hapa, itakuwa pata shika na shaka, nguo kuchanika.
            Si ubishi wala uchawa kukiri kuwa mwaka ulofyatuka tulifyatuliwa na kuufyata bila kufyatuka. Njuluku zilifyatuliwa na maisha yakaendelea kuwafyatua mafyatu waliogoma kufyatua ima kutokana na ufyatu uchwara au kukosa ufyatu kabisa zaidi ya sifa za kipuuzi. Kazi na sifa ya mafyatu ni kama bomu au upinde. Lazima wafyatuke na kufyatua na si kujikomba na kusifia hata ukumbaff. Ila wasipofyatua wakafyatuliwa wanageuka bomu yaani kitu kisichofaa wala kufyatuka na si bomu linalofyatuka na kufyatua. Hata upinde, lazima ufyatuke. Usipofyatuka, hugeuka upondo.
            Sasa turejee na kufyatua inshu ya KAGO na ufyatuaji wa njuluku za mafyatu uliofanywa na mafyatu waliopaswa kufyatuliwa wasifyatuliwe wakaishia kufyatua, bila mafyatu kufyatuka na kuwafyatua hawa mafyatu, watafyatuliwa tena tena hata mwaka huu. Mwaka jana tulifyatuliwa. Mwaka huu tushafutuliwa. Je tutakubali kuendelea kufyatuliwa na wanaotufyatua na kufyatua njuluku zetu au tutawafyatua kabla hawajatufyatua tukafyata na kufyatuliwa kama tulivyofyatuliwa bila kufyatuka bali kufyatuliwa kama tutakavyo fyatuliwa tusivyofyatuka na kufyatua kabla ya kufyatuliwa kwa vile hatufyatuki tukafyatuka? Naona. Hapa nimefyatua hadi mafyatu wanafyatuka kizungumkuti tokana na ufyatu na ufyatuzi wa fyatu mfyatuzi bingwa wa ufyatu na ufyatuzi asiyeufyata wala kufyatuliwa kama mafyatu waufyatao wakafyatuliwa na wale wawafyatuwao wanaopaswa kuwafyatuwa wasiwafyutue.
            Pamoja na KAGO kufyatua ripoti ya ufyatuzi kayani mwaka jana, hadi unaisha, sikuona wala kusikia wafyatuaji wakifyatuliwa na wale wanaopaswa kuwafyatua ili kukomesha ufyatuaji wa njuluku za mafyatu fyata. Pia, kwenye salamu za kuukaribisha mwaka, sikusikia mikakati ya kuwafyatua wafyatuaji wa njuluku za mafyatu. Ajabu, pamona na mafyatua wapaswao kuwafyatua mafyatu wanaowafyatua mafyatu kuufyata, sikusikia mafyatu wakifyatuka na kudai hawa wanaowafyatua wafyatuliwe au wawafyatue hawa wanaopaswa kufyatua wawafyatuao wasio wafyatua!
            Kwanini mafyatu wanaofyatuliwa hawakuwafyatua mafyatu wanaolipwa njuluku kuhakikisha wanasimamia njuluku za mafyata au kuwafyatua wanaowafyatua hizo njuluku wasiwafyatue? Mwaka jana, nilimsikia mwenyewe kwa masikio yangu mtukuka asiyefananishwa na muungu akisema "sababu dosari zilizotolewa hapa, tutakwenda kukaa tuzifanyie kazi, turekebishe na mwakani pengine hizi hazitajirudia, na tutakuwa tumesogea.” Ajabu ya maajabu, katika hutba yake ya kufunga mwaka uliofyatuka, sikumsikia akikumbushia namna atakavyowafyatua hawa wafyatuaji wa mafyatu waliogoma kufyatuka na kufyatua. Je ni kwanini hakufyatuka lau kiduchu juu ya namna atakavyowafyatua hawa mafyatu wafyatuaji wanaohitaji wafyatuzi ili wakome kufyatua njuluku za mafyatu walioamu kuufyata?
            Mwaka jana, tulivyatuliwa matrilioni. Kama wanaopaswa kuwafyatua wanaofyatua mafyatu njuluku wasipowafyatua, sitashangaa KAGO kuja na ripoti kilio cha ufyatuzi wa madafu gizilioni kama siyo quadrilioni. Kwa vile hawa wafyatuaji hawakufyatuliwa na wale wanaopaswa kuwafyatua, sina shaka, watafyatua njuluku za mafyatu tena kama walivyozoea. Kwa kimakunduchi hii huitwa bizinesi ezi usual. Unafyatua hapa na kuhamishiwa pale ili uendelee kufyatua. Kinachoweza kukuzuia kufyatua hapa ni kifo tu. Kama kikufyatua, kila kitu ikiwemo ufyatuzi wa njulu za kaya vinaisha. Ajabu ya maajabu, hata ufyatue vipi, hakuna atakayeondoka na njuluku za mafyatu anazofyatua. Kwa maana nyingine, ni kama unajifyatua kufyatua visivyoweza kukusaidia bwana Godi akikufyatua.
            Japo ukisema haya unaonekana chizi au zwazwa, fyatu ana nini juu ya uso wa ardhi? Ana nini kiumbe aliyekuja bure na kuondoka bure? Laiti mafyatu wengi wangejua ukweli huu, wasingedhulumiana, kuibiana, hata kuuana kwa ajili ya vitu wanavyovikuta na kuviacha hapa. Ukisema ni utaahira, mafyatu wengi wanakushangaa na kuchukia kuwa umewatukana wakati ukweli ni kwamba ni mataahira wasioona zaidi ya usawa wa matumbo na pua zao. Wangapi waliwika dunia hii tena kwa madaraka makubwa lakini walishafyatuka na kusahaulika kiasi cha mali na ushaufu wao kuviacha hapahapa hata wengine kuharibika? Nani hakumbuki fyatu jambazi kama Mobutu Nseleko wa Kongwa alivyojenga kwao kwenye kijiji cha porini cha Gabadolite? Ukiangalia kilichosaliwa baada ya kufyatua na kuunguza njuluku za mafyatu, unakubaliana nami kuwa wanaofyatua njuluku na mali za umma, wengine ni machizi watakaoacha kila kitu hapa wakiondoka watupu kama walivyokuja.
            Wapo wapi akina Mafarao, Nabukadneza na mashaufu wengi uchwara waliojifyatua kwa kuwafyatua wenzao wakidhani hawatafyatuliwa? Tutankhamun, Farao aliyesifika sana, alikuwa na umri wa miaka chini ya 20. Sasa hawa wanaopiga njuluku za mafyatu na kuwafyatua wataishi milele? Unaweza kuacha mijengo mikubwa, akaunti nono, jua kufa ni kufa tu. Heri kuwaneemesha mafyatu kuliko kuwafyatua hadi inafikia mahali unashindwa kujua ni kwanini tumefyatuliwa, tutafyatuliwa,kama hatutachunga kufyatuliwa tena. Hivi niko wapi?
Chanzo: Mwananchi, Machi 24, 2025.

Tunashangaa, Tunashangazwa, na Kushangaza

 

Huwa nashangaa. Sijui kama nawe hushangaa kushangaza? Kama hushangai, unashangaza. Kama unashangaa, pia, unashangaza. Hata nami nashangaza kwa kushangaashangaa bila kufyatua. Huwa nashangaa kwa ninayosikia bila kuona ukiachia mbali ninayoona bila kuyasikia. Katika kaya yetu ya kushangaza, kuna vitu vinashangaza. Kila siku nasikia mafyatu wakilalamikia ukapuku wa kutengenezwa wakati kuna wanene waliofyatua njuluku hadi wanakufuru. Hawa hunishangaa kama nishangaavyo. Tunashangaana, kushangazwa, na kushangaza. Hapa, sijaongelea upigaji wa kutisha kila siku. Unashangaza. Unashangaa kwanini tunapigwa tukaendelea kushangaa hadi tunashangaza. Kwa kushangaa kwetu, tunashangaza na kushangazana. Ukinishangaa, nakushangaa. Usiponishangaa kwa kushangaa, nakushangaa kiasi cha kushangaza kwa kushangaana na kushangazana.

            Siachi kushangaa. Hushangaa kusikia mapambio, mashairi, ngonjera, na sifa tena vya kushangaza. Waimbaji ni mafyatu, wanyama, hata wadudu tena wanaoshangaza. Mfano, wapo waishio kwenye ukwasi wanaoshangaza wanaowashangaa waishio kwenye uchochole wa kushangaza. Licha ya kushangaana, wote wanashangaza. Wapo wanaoshangaa. Wanashaangana na kushangazana. Inakuwaje fyatu awe kapuku kwenye kaya inayosifika kutenda miujiza karibu katika kila jambo? Inashangaza. Wakati wenye njuluku wakiwashangaa wasio nazo, nao wanawashangaa namna walivyozipata wakati wao wakikosa. Inashangaza. Wanashangaa na kushangaza.

Hakuna kitu hunishangaza kama taarifa ya Mkaguzi mkuu wa njuluku za kaya (KAGO). Je huwa kweli anazikagua au zinamkagua? Inashangaza. Kwanza, hizo njuluku ziko wapi na ni kiasi gani? Inashangaza. Pili, kwa zinavyopigwa, sijui kama kweli zipo za kukagua. Inashangaza.  Kwanini asikague hata njuluku za wenye nazo waliozipiga toka kwa mafyatu wnaoashangaa na kushangaza? Nashangaa. Kago anashangaza kiasi cha kumshangaa. Sijui kama naye anajishangaa kwa taarifa atoazo za kushangaza. Je huwa anatushangaa? Kila mwaka, huwa anaripoti upigaji na madudu kibao udhani kazi yake ni kufyatua habari mbaya kwa mafyatu. Inashangaza. Kingine kinachoshangaza ni ile hali ya waliofyatua tena njuluku ndefu kuhamishwa vituo kwenda vingine badala ya kupelekwa lupango. Inashangaza.

 Wakati nikishangaa hili, huwa nashangaa namna Mwendesha Makesi wa Kaya (Dipipii) anavyoweza kukukamatisha, ukapozwa hata kusahaulika lupango halafu anajitoa welewa na kusema eti amekufutia mashtaka. Inanishangaza. Huwa namshangaa na vitu kama hivi vya kushangaza. Je huu muda fyatu wapotezao lupango unalipwa na nani? Inashangaza. Huwa nashangaa kama hii nayo ni haki, sheria, na utawala bora. Juzi, nilimuona mzee Silaha, akiwa amechakaa. Nilishangaa. Alikaa lupango kwa mwezi na ushei. Inashangaza. Ukiuliza nini mbaya alifanya? Unashangaa. Unashangaa ni kwanini ndata walimnyaka na kumsweka lupango bila kupeleka kwa pilato! Unamshangaa yeye kuswekwa lupango bila kosa. Unawashangaa ndata hawashangai hili. Pia, unawashangaa wanene wanaoshangaza kwa kudai kuwa wameleta maendeleo na ustawi. Inashangaza. Hivi vinaweza kupatikanaje bila haki? Inashangaza!

Wakati nikiwashangaa Kago, Dipipii, na ndata wa kushangaza pia, humshangaa munene anayeshughulikia njuluku asifikaye kwa kutoa misamaha ya kodi kwa wenye nazo huku akizidi kuwakamua wasio nazo kwa njia mbali mbali kama vile maokoto, tozos, na madude mengine ya ajabu ajabu na kushangaza. Inashangaza. Kabla ya kumaliza kumshangaa jamaa wa njuluku, huwa nashangaa kusikia kuwa kaya imefunguliwa. Inashangaza. Kwani, nani alikuwa ameifunga na kwanini na ili iweje? Inashangaza.

Hakuna kitu nashangaa kama kukatikakatika kwa umeme. Inshangaza sana kwa namna tunavyoahidiwa kuwa migao ingegeuka historia wakati wowote. Inashangaza namna ambavyo mambo ya kushangaza hutokea na ahadi za kumaliza migao kugeuka donda ndugu. Inashangaza ni kwanini hawa wanaotoa ahadi za kushangaza hawajishangai pamoja na kushangaza! Inashangaza na waathirika wasivyowafyatua. Inashangaza sana kwanini wanaofeli katika kutoa huduma nyeti kama hii kutoachia ngazi ili wenye uwezo waingie na kurejesha heshima ya kaya. Huwa nashangaa. Nashangaa sana kuona kuwa wale wale wanaotudanganya, wanafanya hivyo si mara moja wala mbili. Inashangaza.

Ngoja nifyatue mfano japo mmoja wa kushangaza mjue kwanini nashangaa na kushangazwa.Waziri mkubwa alikaririwa mwaka jana akisema “kwanini Muentertain wizi? Watu wanaiba mara ya kwanza, mara ya pili mmeshindwa kuchukua hatua za kuwadhibiti wasirudie tena?” Inashangaza. Nasikia mafyatu wanafyatua hata pesa ya wagonjwa. Je nini kimefanyika badala ya kulalamika? Inashangaza. Waziri mkubwa, pamoja na mamlaka yake, anashangaa. Inashangaza kweli kweli.

Naendelea kushangaa haya mambo ya kushangaza. Mfano, rahis, akihutubia buge, mwaka 2021 alisema “naomba kutumia jukwaa hili la Bunge lako Tukufu kuwaonya wale wote wanaodhani kuwa usimamizi wa mali ya umma kwa maslahi ya wananchi, kukataa ukwepaji wa kodi, wizi, na kukemea uzembe vitasimama kwa sababu tu Rais Magufuli hayupo.” Inashangaza.

Kwa ufupi ninashangaa, inashangaza, nawashangaa japo mnanishangaa kiasi cha kushangaza na kushangazana kama siyo kushangazwa. Wakati mwingine natamani tuitwe washangaaji kama siyo washangazaji. It’s too much. I wonder.

Ninashangaa kwanini nashangaa! Je wewe unashangaa au unashangaza? Hakika. Tunashangaa, kushangaana, na kushangaza. Mafyatu itikieni ‘kweli inashangaza na mseme amina.

Chanzo: Mwananchi, Machi 12, 2025.

Sunday, 9 March 2025

Sasa Kanji nafyatuka nageuka fyatu dugu yangu!


Juzi natoka Bombei ona mama na toto. Iko furahi kuba sana. Naacha toto moja. Nakuta mama nakwisazaa toto sita. Yote faida. Nakaa Bombei. Woo! heva iko chafu veve hapana ona. Sikia tu. Nalala naota Tanjania. Baada ya peleka faida, sasa narudi tafuta faida nyingine.
        Napanda dege. Nafika hapa. Swahili moja fyatu nataka fyatua mimi. Nalalamika kama toto eti fyatu fyatuzi iko nafyatua mimi hadi nafyatuka! Swahili nakuta mimi iko soma gazetini. Nauliza kwanini juluku naibiva kila siku? Nasikia hii iko chava. Kama nasema baya sirkal, nachukia veve. Kwanja, naanja. “Hii hindi iko chafu nachanganya Swahili sana. Napenda sana siasa na iko na multiple citizenship.” Nalalamika eti hapana piga kura lakini kama ongozi nachaguliwa, yeye nakaribisa na kuwa karibu nayo. Naongeza kuva Kanji nafanya ongozi sahau ile nachagua yeye. Sasa iko kosa ya yangu au ongozi? 
        Hii jinga naita mimi choli! Lini swahilihindi nakuwa safi dugu yangu? Kama nafyatua hindi nachanganya na Swahili nafanya juli sana. Naondoa baguzi ya luga na rangi dugu yangu. Sasa kosa nini veve nataka fyatua mimi dugu yangu? Mimi iko penda veve sana na juluku yako naleta dukani yangu nunua witu. Vote napata faida. Veve chukua witu. Mimi chukuva juluku. Hapana pendeja hiyo dugu yangu?
Nafika jumbani. Nakuta Swahili nalalamika sana. Nauliza “iko nini veve nalalamika owo kama toto dogo? Swahili iko sangaa kama paka naona juluku! Nauliza tena. Veve napata sida gani nasangaa hiwi? Nasema eti mimi hapana ongea Swahili juli. Nasangaa hadi nataka fyatua Swahili. Nauliza yeye “kwani Swahili iko ongea hindi juli? Sasa Swahili nataka fyatua kila kitu. Nataka hata kuoa totoz ya hindi! Kwanini nakuwa chokoji? Veve iko ona hindi naona totos ya Swahili? Sasa kama siyo nafyatuka, kwanini taka oa totos ya hindi veve Swahili choli?
        Swahili iko tabu mingi sana. Maisha iko gumu au fyatu iko gumu fyatuka na kufyatua ile nafyatua yeye? Naona vatu ikolalamika maisha iko gumu kama jiwe. Kwani, swahili siyo gumu? Swahili nalalamika kama toto dogo. Hindi nalalamika kama vatu kuba. Kama maisha nakuva gumu, kwanini hapana fyatua ile nafanya maisha kuwa gumu? Sasa lalamika nageuka sera ya vatu vote kwa kayani. Hindi nalalamika. Sirkal nalalamika. Tajir na sikini yote lalamika! Kama sirkal nalalamika, nan tasaidia nani? 
            Maisha iko gumu. Sasa hindi nafatyatuka nageuka fyatuzi dugu yangu. Sasa nauliza polepole. Juluku kayani nakvenda vapi? Mbona ile kuba naishi peponi? Kama Swahili napata juluku, naoa vake mingi. Hii hapana lalamika! Natumia juluku mingi fanye serehe. Juzi nakwenda Bembei. Kule jimboni yangu India, vaziri moja ya koa nasamehe juluku rupia laki moza nafukujwa kaji. Hapa vaziri nasamehe, trilioni napandishwa choo! Sasa hapa laumu nani na nini dugu yangu? Kvanini hapana fyatuka ikafyatua ile nafyatua veve dugu yangu?
Svahili iko tabu sana. Nakwenda sule. Napata digrii mingi. Hapana fanya biasara. Naogopa hasara lakini naishi kwa hasara. 
        Swahili iko penda faida. Vapi tapata faida kama hapana biasara? Au nataka kwenda kwa sirkal na kuibia chofu na fyatu juluku? Ile nasoma nayo howo kabisa. Napata digrii ya chumi nakuja chuma chovu na fyatu! Ile napata kazi kwa sirkal nageuka fisadi kuba. Kama hindi nasindva kwepa kodi, hapana lalamika. Hapa svahili nalalamika. Nasema hindi fisadi kuba. Kwani, hindi dio naongoza kayani?
         Sasa sirkal kama nalalamika hapana juluku, kvanini nasamehe kodi ile fanyabiasara kuba kuba? Hapana ona nafyatua na kuumija vatu yake? Nasikia kwa bungeni vaziri naulizwa kwanini nasamehe kodi bila kufuata sharia. Yeye nanyamaza kama jusi nabanwa na lango au chura kuba!
Sasa fyatu vote nakaa kimya hapana fyatukia vaziri lakini nafyatua kelele tu! Napiga kelele mingi kama chura ya bawani. Chura iko imba “yangu yangu.” Kama naokota jive napiga yeye, nakimbia! Natoka bawani hapana guo ya mvilini. Mingine naita chava. Naitwa chava nafurahi! Chava iko dudu chafu. Iko dogo na howyo sana dugu yangu. Je Swahili natofautina na chava guoni na chura bawani? 
        Kama nataka pata juluku, napasa kwenda fyatua ile fyatu kuba nafyatua juluku yao. Napasa zuia choli na mizi kuba. Kama naiba juluku na fyatu naomba yeye saada, sasa taacha kuiba juluku? Hapana nunua gari mingi ya sirkal. Naharibu kusudi. Nanunua vatu kuba kuba. Nakaa jumbani kuba kuba. Naoatesa tumbo kuba kuba. Naitwa kuba. Kila kitu ya kuba, kuba tu. Sasa dogo naishi vapi na wipi? Hapana tumia gari ya sirkal sereheni. Hapana nasafiri sana. Hapana fanya sanii na babaisaji mingi mingi. 
Kama nafanya mambo kuba na veve iko dogo na akili dogo, hapana ona naleta balaa na fyatu mingi nakosa juluku hadi nafyatuka nataka kufyatua veve kwa sababu ya jinga yako na akili dogo? Du! Kumbe naota!!
Chanzo: Mwananchi Alhamis iliyopita.

Chunga yasikukute ya Aziz na ndoa ya majuu

Aziz ni kijana wa miaka 24 wa Kipalestina aliyekimbia udhalilishaji kwao akaishia kudhalilika majuu. Kisa cha Aziz kinafikirisha, kusikitisha, na kufundisha. Wapo wengi kama Aziz walioharibikiwa maisha baada ya kuolewa wakidhani wameoa majuu. Kijana huyu, akiwa hajui hata Kiingereza, alijikuta akijiingiza kwenye ndoa ya mateso. Nkwazi alimjua Aziz. Alikuwa rafiki wa kaka yake aliyemlalamikia kuwa mdogo wake alikuwa akipoteza mwelekeo.
Tokana na kuwajua wote wawili, Nkwazi aliamua kuingilia kati kumsaidia Aziz. Kaka mtu aliwakutanisha Aziz na Nkwazi nyumbani kwetu walikozoea kuja kupoteza muda na kufundishwa Kiingereza. 
        Baada ya kaka mtu kueleza kisa kizima mbele ya mdogo wake, kama marafiki na walezi, tulimuuonya Aziz asijiingize kwenye uhusiano ambao ungemletea majuto baadaye. La kufa halisikii dawa. Azizi alichukia hadi kutwambia “hii ni Kanada nchi huru ambapo kila mmoja anaweza kufanya atakavyo.” Kwa maneno mengine, alitaka tusimuingilie katika maisha na uhuru wake hasa ikizingatiwa kuwa Kanada, vijana huweza kuamua kufunga ndoa hata bila kuwahusisha wazazi na ndugu japo si wote. Ghafla, Aziz aliacha kuja kwetu. Tulijua sababu. Aziz alikuwa kwenye mapenzi na mama aliyemzidi umri tutakayemuita Meg japo si jina lake aliyetaka wafunge ndoa. 
Pamoja na kumuonya asisikie wala kujali,  tulijua ni haki yake kufanya hivyo japo tulimtahadharisha juu ya tofauti za mila na dini. Mfano, tulimjua Meg kama mama aliyekuwa amempenda akipanga kufunga naye ndoa, alipenda sana kuongelea mbwa wake ambaye alikuwa akisema kuwa hata hula na hulala naye wakati mwingine. 
        Si ajabu huku kwa baadhi ya watu kula na mbwa kwa sababu kwao, mbwa ni sehemu ya familia. Hivyo, tuliona hatari itokanayo na kutofautiana kidini na kimila ambavyo vingemkwaza Aziz japo hakusikia. Baada ya kugundua kuwa Aziz alianza kutuchukia mbali na Meg ambaye alikuwa ameambiwa juu ya ushauri wetu, tulimuacha. Maana, yalikuwa ni maamuzi na maisha yake.
Hakika, Aziz na mama wa Kizungu walifunga safari kwenda kwenye visiwa vya Saint Lucia na kufunga ndoa na Meg.doa ilifungwa. Ndoa ilifungwa na fungate ikafanyika. Aziz na Meg walirejea Kanada wakiwa mke na mume. Baada ya muda mfupi, tuliamua kuhama mkoa tuliokuwa tunaishi na kusahau mambo ya Aziz na Meg.
Siku moja, Nesaa alikwama kwenye theluji usiku akitoka shule. Alijitokeza baba mmoja wa Kiarabu aliyekuwa na familia yake akamsaidia kwa kujaribu kukwamua gari asifanikiwe. Hivyo, alishauri ampe lift hadi nyumbani. Yule baba alimfikisha Nesaa nyumbani. Tuligundua kuwa kumbe aliishi mtaa wa pili toka kwetu. Alimsaidia Nkwazi kukwamua gari na tangu siku hiyo wakawa marafiki.
Baada ya miezi kupita, yule Mwarabu alikuja kutuaga kuwa alikuwa anahamia Toronto. Tulifurahi sana na kusikitika. Hata hivyo, alituuliza kama tunamjua Aziz toka kule tulikokuwa tukiishi mwanzo. Alituelezea namna Aziz alivyomuomba atuombe msamaha kwa kudharau ushauri wetu.             Tulimuuliza yule Mwarabu sababu za Aziz kukimbia na kujutia ndoa yake. Alitwambia kuwa Meg hakuwa tayari kubadili dini wala kuheshimu mila ya Aziz mbali na kutokuwa tayari kuacha kufuga mbwa wake kipenzi pamoja na mambo mengine binafsi kama nani mwenye madaraka zaidi ya mwingine kati yake na mkewe. 
        Kwa ufupi, Aziz alijikuta kwenye ndoa ya mateso hadi akakimbilia Toronto kuepuka ndoa ya mateso. Tulifurahi kusikia kuwa Aziz alikuwa amegundua makosa yake na mchango wetu na kujutia. Hata hivyo, maji yalikuwa yameishamwagika. Aziz, licha ya kuonja mateso na kuumia, alipoteza malengo na muda wake. Kwani, tulimshauri akasome kwanza akaghairi. 
Sasa tujiulize. Kisa hiki kinafundisha nini? Mosi, usilolijua litakusumbua hata kukuuumiza. Pili, asiyesikia la mkuu huvunjika guu. Tatu, vijana waepuke kujiingiza kwenye makubaliano ya ndoa bila uzoefu wala ushauri.
        Nne, tofauti za dini hata mila ni muhimu katika kufikia maamuzi ya kufunga ndoa. Mfano, Aziz, muislam, asingeweza kuishi na hata kuchangia kitanda na vyombo na mbwa.
        Tano, umri katika ndoa ni muhimu. Japo hatukatazi waliozidiana umri kuoana, kuna haja ya kulidurusu na kulijadili hili kabla ya kujifunga kwenye ndoa. 
        Sita, si kila ving’aravyo ni dhahabu.
saba, ingawa haya yanaweza kuchukuliwa kama masuala binafsi, yana somo kubwa kwa vijana wanaofikiri kuwa kuoa majuu ni kuukata. Wakati mwingi na mwingine, kufanya hivyo si kuukata bali kukatwa kama ilivyo kwa Aziz na wengine kama yeye.
Chanzo: Mwananchi Leo J'pili.

Wednesday, 26 February 2025

No reforms, no elections ilhali tushageuzwa na kuchakachuliwa!!

 

Mjini hakuna stori ya no reforms no elections, kwa kisambaa, hakuna mageuzi, hakuna uchaguzi. Kwanza, sijui kama mafyatu waliofyatuliwa na shida wanaweza kufyatuka wakawafyatua wawafyatuao. Wapo wanaosema eti mafyatu watinge mitaani na kukinukisha! Loo! Mbona mwaota mchana! Mnategemea mafyatu waliofyatuliwa wakafyata wafyatuke watekwe na kupotezwa? Nani afyatuke afyatuliwe shaba kama Tunda Lishe? Waliokwishatekwa, kuteswa, na kupotezwa watoshe. Nasikia ngebe za mageuzi kutaka uchaguzi huru na wa haki. Nani kawambia duniani kuna haki au uhuru hasa kwa mafyatu wafyatuliwa? Hamjaambwa kuwa haki hupokwa na iko peponi au motoni? Acheni ufyatu. Mkikomaa, nateka na kupoteza mkapate haki huko mtakakoharakishiwa. Siwatishi au kufyatuka kifyatu. Wangapi weshatekwa na kupotezwa? Nini kimefanyika?
            Tukiwa wakweli, lini mliwahi kuwa na uchaguzi huru na wa haki au mnaita uchakachuaji uchaguzi? Mnataka kumfyatua nani? Uchaguzi ni dhana tata. Unaweza kuchagua hata kuchakachua ukajiaminisha umechagua. Waweza kutochagua ukapitisha bila kupingwa ukajiridhisha umechagua japo hukuchagua. Mnataka mageuzi. Nani anataka kugeuzwa kama pweza kikaangoni ilhali walaji weshajiandaa kumfyatua hata bila kumpika au kumgeuza?  Kubalini yaishe. Baada ya wenye kaya kufyatua na kupitisha ‘mpendeka na mkubalika’ bila kupingwa hata walipotaka kumpinga, wapingaji wamefyatuka. Wanataka wamfyatue kupitia mageuzi. Wanafyatuka eti watasusa uchakachuaji. Ebo! Mkisusa, wachakachuaji watachakachua, kufyatua, na kula. Mmesahau mazoea au mwajitoa akili? Mnakuwa kama hamjui inshu mafyatu wangu! Kwa taarifa yenu, hata muwange uchi, hakuna cha haki wala mageuzi.
            Mafyatu wangu mlofyatuka na kutaka kufyatua, mnataka kujifanya hamjui manufaa ya kupitisha bila kupingwa kwa kaya na mafyatu waliofyatuliwa wakagoma kufyatuka na kufyatua!? Nazoza na mafyatu mliofyatuka mkatishia kususa uchakachuaji. Kwani hamjui kuwa mpakwa mafuta aliyepitishwa bila kupingwa lazima apite, apete, na kutesa hata mkisusa? Nyie mafyatu msiofyatuka hadi mkafyatuliwa nani aliwaroga kudhani kuwa mageuzi yanaweza kuleta mageuzi ilhali gegezi? Mkitaka mageuzi, jigeuzeni mfyatuke muache kufyatuliwa. Haki haiombwi, hupokwa. Hivyo, kususa ni kusuasua na kufyatuliwa. Badala ya kusema no reforms no elections mseme we must fyatuka and fyatua them to grab our rights. Period.
            Tukubaliane hata kwa kupingana. Mnapingaje mteule wa Mungu mwenye maono na ndoto visivyo vya kifyatu? Hamjui kuwa wateule wa Mungu hupaswa kutawala milele kama Ngwazi wa kwa akina Bwinobwino? Hamuoni maajabu yalotendwa kama ‘kufungua’ kaya iliyomkuwa imefungwa kwa makufuli japo ‘mfunguaji’ alikuwa na walioifunga, kama kweli ilikuwa imefungwa? Sasa kaya ‘imefunguliwa.’ Mnataka nini kama siyo ufyatu uchwara unaowafyatua? Mnapingana na kazi ya Mungu iliyomuondoa Jiwe. Eti mwataka kitabu, sijui katibua, sijui katiba! Mshaambwa kitabu mnachotaka kibadilishwe ni makaratasi yasiyoweza kuzuia mteule kupeta hata kwa goli la mkono.
            Kwa vile kimeishaumana, ishajulikana. Mafyatu weshafyatuliwa wakafyata wasifyatuke. Napendekeza tuokoe njuluku za mafyatu. Tusifanye uchakachuaji, sorry uchaguzi. Isitoshe, tukipitisha mpakwa mafuta tena bila kupingwa na kupingana, tutaondoa hatari za kutekana na kupotezana. Kwa vile ‘anakubalika’ kwa kila kiumbe, mafyatu, ndege, hata wadudu kama chawa na kunguni waliotamalaki siku hizi tokana na maajabu na miujiza, nasema kwa kinywa kipana tena kwa herufi kubwa HAKUNA MAGEUZI. No chakachuaization. Si inampendeza?
            Wasusaji, chonde chonde. Msituvurugie amani kupinga visivyopingwa au kutaka kugeuza visivyogeuzwa. Mnadhani waliofyatuliwa wakapitisha hawakufanya mageuzi? Unaweza kufanya mageuzi bila mageuzi na yote ni mageuzi. Kama mligeuzana na kupinduana, hayo hatutaki. Mnadhani mlivyochafuana na kuvuana nguo, mngekuwa na dola, si mngetekana na kupotezana? Shukuruni hamna dola. Mafyatu tunataka mapinduzi si mageuzi. Mapinduzi huleta amani. Mageuzi huleta machafuko. Nani anataka shari? Kawaulize wenzenu wa kaya ya jirani waliofanya mageuzi. Kila siku, wanageuzana hadi inakera. Wamegeuzana hadi wakawageuka mafyatu. Najua wapingaji hamjakaribishwa kufyatua keki ya kaya. Hivyo, mwawaonea maya tu. Kwa anayetaka mageuzi, anapaswa kupoka haki ndo aje na lugha ‘isiyokubalika’ ya mageuzi. Mnageuza nini wakati tulishageuzwa tangu zama za zidumu fikra za mkiti? Anayebisha aniambie. Lini tulifanya uchaguzi zaidi ya uchakachuaji na uchaguzi?
         Mcheke, mnune, mfyatuke, mfyate, mzoze, mzuzuke hata kuzomea, lazima mpakwa mafuta apite kama alivyoingia. Sasa mnafyatukafyatu ili iweje? Ufyateni na kukubali kufyatuliwa au mfyatuke mfyatue tujue. Kwanini kutaka kugeuza ‘mageuzi’ makubwa ya kidemokrasia yaliyokwishafanyika? Nani haoni haya mageuzi na maendeleo? Kama mnayaona, basi yakubalini tuendelee kutesa pasina kutesana au kuteseka na mageuzi. Kama hamuyaoni, jifanyeni mnayaona. Kama hayapo, jifanyeni yapo, na kama hayafai, jifanye yanawafaa hata kama hayawafai. Mwataka tuwakaubalie mgeuze mipango iliyopitishwa bila kupingwa? Machawa, sorry mafyatu weshasema liwalo na liwe.
Lazima mpakwa mafuta wao apite. No fyatuka, no fyatuliwa. Nisisiteze. Unaweza kuchagua kwa kutochagua na kutochagua kwa kuchagua. Yote ni uchaguzi na uchaguzi ni demokrasia hata kama ghasia. Wanaotaka mageuzi, wangoje hadi Yesu arudi. Hivi leo nimekunywa ngapi?
Chanzo: Mwananchi Leo.